Wednesday, March 18, 2015

Nyalandu ampiga kijembe Kinana



Wednesday March 18, 2015

Na Veronica Romwald, Dar es Salaam

WAZIRI wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu jana alionekana kumpiga kijembe Katibu MKuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Abdulrahman Kinana aliposema kuwa sasa atakuwa anazurura angani.
Nyalandu alitoa kauli hiyo Dar es Salaam alipozindua ndege nyepesi (Micro-Light, 5H – Hel), ambayo itatumika kupambana na ujangili katika Hifadhi ya Taifa ya Selous.
“Karibuni wote, leo tunazururia hapa uwanja wa ndege na ninazindua ndege hii nyepesi ambayo imetengenezwa Ufaransa, itatumika kupambana na majangili katika Mbuga ya Selous.
“Kwa maana hiyo sasa tunaanza kuzururia angani kupambana na majangili na nasisitiza kwamba ndege hii ni mpya kabisa na gharama za uendeshaji wake ni ndogo kwa vile inatumia petroli,” alisema.
Hivi karibuni Kinana akiwa ziarani mkoani Arusha alimsifia Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa (CCM) kuwa ni mchapakazi lakini Waziri Nyalandu ni mzururaji.
Akizungumza jana wakati wa uzinduzi wa ndege hiyo ya kupambana na ujangili, Nyalandu alisema imetengenezwa kwa gharama ya Dola za Marekani 2,040,000 na ina uwezo wa kubeba askari mmoja na rubani.
Waziri Nyalandu alisema ndege hiyo imeundwa kwa usalama wa hali ya juu kwa kuwekewa puto (parachute) ambalo litatumika kushuka chini iwapo ndege itaishiwa mafuta angani.
“Itakapoanza kutumika itasaidia kuwabaini majangili, inakwenda kwa mwendo mdogo iwapo angani hali ambayo inawezesha kuwaona majangili na kila kinachoendelea ardhini kwa wepesi,”alisema Nyalandu.

No comments:

Post a Comment