Saturday, December 14, 2013

Majengo muhimu yaliyobaki historia Kilwa Kisiwani


Jengo la Serikali ambalo pia lilitumika kama ngome ya gereza ya Kikoloni enzi hizo. Picha na Maimuna Kubegeya 
Na Maimuna Kubegeya, Mwananchi

Posted  Decemba14  2013 
Kwa ufupi
Tofauti na miji mingine ya kale mji wa Kilwa Kisiwani ulikuwa kiunganishi na kitovu kikubwa cha biashara kati ya watu wa Bara la Afrika, Bara Asia na kwengineko. Historia inaonyesha kuwako kwa majengo kadha wa kadhaa yaliyoacha historia kubwa duniani.
Kilwa. Mji wa Kilwa Kisiwani Mkoani Lindi ni miongoni mwa miji michache iliyobeba historia ya Bara la Afrika. Inasadikiwa kuwa mji huu ulianza katika karne ya saba baada ya Kristo takribani miaka 1,400 iliyopita.
Tofauti na miji mingine ya kale mji wa Kilwa Kisiwani ulikuwa kiunganishi na kitovu kikubwa cha biashara kati ya watu wa Bara la Afrika, Bara Asia na kwengineko. Historia inaonyesha kuwako kwa majengo kadha wa kadhaa yaliyoacha historia kubwa duniani.
Katika makala zilizotangulia tuliona baadhi ya urithi wa kihistoria ulioachwa katika eneo hili la Kilwa Kisiwani. Nikiwa mmoja kati ya watu waliobahatika kufika kwenye mji huu, nilishuhudia vituo 10 muhimu vinavyopatikana Mafia Kisiwani.
Vituo hivyo ni majengo muhimu yanayoendelea kuwapo hadi sasa yakithibitisha kuwapo kwa vizazi vilivyokuwa vikiishi eneo hilo kama ifuatavyo;
Makutani Palace
Neno Makutani lilimaanisha eneo lenye kuta kubwa. Eneo hili lililokuwa limezungushiwa ukuta mrefu. Ndani ya eneo hili kulikuwa na majengo mengi. Pia lilikuwa ni eneo alilokuwa akiishi Mfalme Hassan bin Ibrahim, aliyekuwa akijishughulisha na biashara. Ni eneo lililo upande wa Mashariki mwa Kisiwa cha Kilwa.
Msikiti mdogo
Hatua chache kutoka eneo la Makutano kuelekea upande wa Magharibi mwa Kisiwa hiki, kuna jengo la msikiti uliokuwa miongoni mwa misikiti 99, iliyopatikana ndani ya Kisiwa hiki kwa wakati huo. Msikiti huu ulijengwa katika karne 15 na sasa una takriban miaka 600.
Msikiti mkuu
Unapomaliza eneo la msikiti mdogo, unaingia kwenye eneo lililo na msikiti mkubwa. Msikiti huu unatajwa kuwa mkubwa zaidi katika karne ya 11 kuwahi kujengwa Kusini mwa Jangwa la Sahara. Msikiti mkuu ni misikiti miwili iliyounganishwa pamoja. Ndani yake kuna ukumbi wa kuswalia na unasadikika kuwa ulijengwa tangu karne ya 11. Pia kuna uwanja wa kutawadhia, wenye mabirika ya maji na mawe laini ya kufutia miguu.
Ukumbi mkubwa zaidi wa kusalia na sehemu kubwa zaidi ya kutawadhia vilijengwa takribani miaka 1,320. Sultani Al Hassan Bin Sulaiman anatajwa kuhusika na ujenzi wa msikiti huu. Ndani ya msikiti huu kuna chumba maalumu alichokuwa akiswalia Sultani.
Ngome ya Gereza
Hatua chache kutoka msikiti mkubwa kuna jengo kubwa linalofahamika kama Ngome ya Gereza. Tofauti na majengo mengine, jengo hili halikujengwa na wakazi wa Kilwa, bali lilijengwa na Wareno, walioongozwa na Fransisco De Almeida.
Lengo kuu la ujenzi huu ilikuwa ni kupata eneo litakalotumika kama ngome ya ulinzi itakayotumika kuona maadui kabla ya kufika ndani ya kisiwa hicho.
Jengo hili lilijengwa katika karne ya 15, Ikiwa ni ngome ya kwanza kuwahi kujengwa na Wareno katika Pwani ya Afrika Mashariki, wakati huo Wareno hao walijaribu kudhibiti maeneo mengi ya Pwani wakilenga kudhibiti pia biashara ya za maliasili, hasa madini yaliyokuwa yakipatikana katika maeneo hayo.
Ngome nyingine zilizojengwa na Wareno katika karne hiyo ni pamoja na Ngome Kongwe ya Zanzibar, Fort Jesus ya Mombasa nchini Kenya na Fort Sao Sbastiao ya Beira Msumbiji wakati ule ikijulikana kama Sofala.
Msikiti na makaburi ya Malindi
Majengo ya msikiti huu yalijengwa katika karne ya 15 na kufanyiwa marekebisho katika karne ya 18. Yanapatikana hatua chache ubavuni mwa Ngome ya Gereza. Pembeni ya msikiti huu kuna makaburi ya wanafamilia walioishi katika kisiwa hicho waliokuwa na asili ya Kenya.
Makaburi hayo yanafanana na makaburi mengi ya Kisultani yaliyokuwa yakijengwa katika karne hiyo kwenye maeneo mbalimbali hasa Pwani.
Husuni Kubwa
Umbali wa kilometa mbili kutoka makaburi ya Malindi. Linapatikana jengo kubwa zaidi kuwahi kujengwa Kusini mwa Jangwa la Sahara katika karne ya 14 hadi 15. Likiwa na vyumba 100, mabwawa ya kuogelea, kumbi za mikutano na kumbi za kufanyia biashara. Jengo hili lililojulikana kama Husuni kubwa lilijengwa katika karne ya 18. Sultan Al- Hassan Bin Sulaiman ndiye hasa aliyefanya ubunifu huo.
Husuni kubwa lilikuwa jengo la ghorofa lililo kando ya Bahari ya Hindi. Ni jengo lililotengenezwa kwa mawe na chokaa, likiwa na mapambo ya kila aina kama yalivyobiniwa na wasanifu wa majengo wa wakati huo
Husuni ndogo
Jengo hili linapatikana pembezoni mwa Husuni Kubwa. Ni miongoni mwa majengo yaliyoharibika zaidi, kwani kwa sasa linaonekana sehemu yake ya chini pekee ambayo ni msingi mkuu wa jengo hilo.
Inaaminika kuwa jengo hili liliwahi kuwapo kabla ya kujengwa kwa Husuni kubwa. Kwa mujibu wa wataalamu wa mambo ya historia, Husuni ndogo ilijengwa kati ya karne ya 12 na 13.
Inasadikika kuwa ndani ya jengo hili kulikuwa na stoo kubwa iliyotumiwa kuhifadhi madini ya dhahabu, pembe za ndovu na vitu vingine vya thamani kwa ajili ya biashara.
Makaburi ya Sultan
Hili ni eneo kubwa la makaburi lililopo ndani ya kisiwa hiki. Makaburi mengi yaliyopo katika eneo hili ni ya viongozi mbalimbali waliowahi kuishi ndani ya kisiwa hicho tangu karne ya 16.
Ushahidi unaonyesha kuwa kuna makaburi mengine yaliyojengwa katika karne ya 17, 18 na 19.
Mengi ya makaburi haya yameandikwa kwa lugha ya Kiarabu, jambo linalothibitisha kuzikwa kwa watu wenye asili ya Uarabuni, waliokuwa wakiongoza na kujulikana kama masultani.
Mabaki ya majengo ya makaburi hayo, yanapatikana hadi leo. Hii ndiyo Kilwa Kisiwani.

No comments:

Post a Comment