MLIMA Kilimanjaro umelijengea heshima kubwa
taifa la Tanzania ukiachilia mbali mapato yanayopatikana kutokana na wageni
wanaofika kupanda mlima huo.
Mlima huu ambao una urefu wa mita 5,895 (futi
19,340) unachangia zaidi ya asilimia 40 ya pato la taifa, huku kila mwaka
mapato yanayotokana na utalii wa Mlima Kilimanjaro ni zaidi ya sh bilioni
80.
Licha ya mapato makubwa yanayotokana na mlima
na fursa ya ajira, kuna hatari ya kutoweka kwa mlima huo, kutokana na
theluji ya mlima kuendelea kupungua na kuwapo kwa moto ambao umekuwa
ukiwaka na kuchoma misitu ya asili karibu kila mwaka.
Ripoti mbalimbali za tafiti juu ya hali ya
Mlima Kilimanjaro zimekuwa zikifanywa na kueleza hali mbaya ya mlima
hususan theluji ya mlima kutoweka.
Mmoja wa watafiti, Jacques Blot wa Chuo Kikuu
cha Bordeaux, Ufaransa kwenye moja ya tafiti zake anasema tangu mwaka 1912
theluji ya mlima imepungua kwa zaidi ya asilimia 80.
Ripoti nyingine zinaeleza kuwa theluji ya
mlima ilikuwa kwenye maeneo sita yenye barafu lakini sasa ni maeneo matatu
pekee yaliyobaki.
Licha ya kuwapo kwa sababu za asili ambazo
zimechangia kupungua huko lakini pia kuna sababu nyingine zinazotokana na
uzembe wa kiutendaji wa viongozi wetu.
Ilikuwa Julai 7, mwaka huu nilipopokea simu ya
mwananchi mwenye uchungu na nchi hii akisema eneo la kaskazini mwa Mandara
katika Mlima Kilimanjaro moto mkubwa unawaka.
Eneo lenye ukubwa wa ekari 40,000 liliteketea
kwa moto.
Kwa mujibu wa Mkuu wa Idara ya Mahusiano na
Mawasiliano wa Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (Tanapa), Pascal
Shelutete, anasema kuibuka kwa moto huo si mara ya kwanza kwani mwaka 2009
eneo lenye ukubwa wa kilomita za mraba 70,000 pia ziliteketea kwa moto.
Tangu miaka ya 1960 Mlima Kilimanjaro umekuwa
ukiwaka moto, lakini licha ya madhara yake kwa miaka hiyo, si kama ilivyo
sasa, ambapo kuna uhaba wa mvua na unyevu, hivyo lazima madhara yawe
makubwa.
Mlima Kilimanjaro unaozungukwa na halmashauri
za wilaya sita; Siha, Hai, Moshi Vijijini, Moshi Mjini, Rombo na Same,
licha ya kuzalisha mapato mengi lakini wananchi wanaouzunguka mlima huu
hawanufaiki, wengi wao ni maskini.
Lakini viongozi wa hifadhi wamebaki kushikilia
kuwa mahusiano ni mazuri na wanaendelea kuimarisha mahusiano huku mambo
wanayozungumza yakiwa kwenye maneno na maandishi lakini wananchi
hawanufaiki kwa lolote.
Wananchi hawaoni faida yoyote ya kuwa karibu na
mlima, wengine wanadiriki hata kutosaidia shughuli za kuzima moto, hivyo
utaona ni jinsi gani itakuwa vigumu kwa hifadhi kuendelea kubaki salama na
kupambana na vitendo vya uharibifu wa mlima.
Mlima Kilimanjaro una eneo kubwa na msitu
mnene; ni dhahiri kuwa kwa kutokuimarishwa kwa ujirani mwema lazima vitendo
hivi vya moto vitaendelea na hatimaye mlima huu barafu itakwisha pamoja na
uoto wa asili na kubaki jangwa.
Tatizo jingine ni kutokuwepo kwa mahusiano
mazuri kati ya majirani wa mlima na askari ambao wamepewa jukumu la kulinda
mlima huo.
Najua Tanapa wanatekeleza wajibu wao ila kwenye
vijiji vingi nilivyopata fursa ya kutembelea kuna umuhimu wa kuwachukulia
hatua askari ambao wamekuwa wakilalamikiwa kuwafanyia wananchi vitendo
ambavyo si vya kibinadamu wanapowakuta wameingia kwenye hifadhi.
Hushangai kukutana na mwananchi, tena mwanamke
akakuambia amekutwa na askari wa Hifadhi ya Kilimanjaro (Kinapa)
akikata majani akalazimishwa ale majani.
Sisemi wananchi wavunje sheria zilizopo, la
hasha! Ila sheria ichukue mkondo wake, hata kama mtu amevunja sheria pia
ana haki ya kuwajibishwa kwa kutumia sheria aliyoivunja na si kumuwajibisha
utakavyojisikia.
Kinapa ijitazame upya katika hili, kwani
vitendo hivyo vikiendelea vya ukatili kwa wananchi ambao ndio wanaoishi
karibu na mlima kuliko askari wachache ni dhahiri kuwa lazima vitendo vya
uharibifu vitaendelea.
Kwanini hatuwezi kujiuliza ni kwanini tangu
tunapata taarifa za moto haujawahi kuwahiwa kuzimwa bila kuteketeza ekari
nyingi?
Tanzania yetu tunaijua na viongozi wetu
tunawajua, wakizungumza ni kama malaika, lakini matendo yao hayaendani na wanachozungumza,
hivyo ni vema Kinapa ikaimarisha mahusiano ya ujirani mwema ili wananchi
waone faida ya kuwa karibu na mlima kabla ya kuchukua hatua nyingine.
Hivi sasa wizara ndiyo inaona umuhimu wa
kuanzisha mfuko wa kuulinda Mlima Kilimanjaro dhidi ya majanga ya moto,
yaani utafikiri moto umeanza mwaka huu, ambapo tunarudi palepale kwa
niliyoyazungumza, kwani mpango huo utategemea wananchi katika vijiji
vinavyozunguka hifadhi, ambao wametelekezwa na hawaoni faida ya kuwa karibu
na hifadhi, hivi kweli tutafanikiwa? Tunapaswa kujiuliza.
|
No comments:
Post a Comment