|
WAZO
binafsi ni kuamini kuwa kama kuna utatu mtakatifu, mfano wa ule wa mbinguni,
basi utatu huo mtakatifu kwetu Tanzania ni Ikulu, Mahakama na Bunge tukufu,
mahali ambapo hakika panasimamia na kuwakilisha mamlaka, haki na usawa ili
kudumisha amani nchini.
Wakati
tukiwa na taasisi hizo ‘takatifu’ hususan Bunge, tena moja, lenye wajibu
muhimu wa kutunga sheria na kuisimamia Serikali katika kutekeleza majukumu
yake kwa wananchi kumezuka minong’ono kwamba baadhi ya wawakilishi wetu hao
wamegeuka kuwa ‘watetezi’ wa watuhumiwa mbalimbali likiwamo hili la ujangili
tena ndani ya chombo cha kutunga sheria!
Zipo
taarifa mbalimbali zinazonukuliwa na vyombo vya habari kama vile: ‘Ujangili
kulitesa Bunge’ na kadhalika; na wabunge kukinzana vikali huku suala la
ujangili likifahamika wazi wazi miongoni mwa Watanzania kuwa ni moja ya
tuhuma za makosa ya jinai kwa mujibu wa sheria zetu hizo hizo zilizotungwa na
kupitishwa na Bunge letu.
Kama
hivi ndivyo, ni kwa vipi sasa katika suala hili la ujangili ambalo ni tuhuma
nzito ya uhalifu linazusha kuwepo kwa pande mbili kinzani bungeni, moja ikiwa
mtetezi mkuu na kwa kauli za hisia kali hasa baada ya upande mwingine kutoa
taarifa na hata ushahidi wa awali kwa wahusika wanaojihusisha wakiwamo wale
walionaswa.
Wazo
jepesi na mtazamo wangu ni kuwa hawa ‘watetezi’ wanaotumia kauli kubwa, nzito
na za hisia kali kuwatetea hata baadhi ya watuhumiwa walionaswa na vyombo
vingine vya dola katika ujangili hakika hawawatendei haki Watanzania na
vyombo vingine husika vya dola na wala utetezi huo haujengwi kwa kuzingatia
msingi wa utawala bora, kwani zipo mahakama ambapo ni mahali mahususi kwa
utetezi kama huo kwa wahusika.
Pasipo
shaka utetezi kama huo ambao huenda hauzingatii misingi ya utawala bora,
yaani wa kuzingatia mifumo ya sheria unaweza kutengeneza na kuzusha hisia
miongoni mwetu wananchi tunaowakilishwa kwamba pengine watetezi hao wana
masilahi binafsi katika suala la ujangili na si bure.
Kwa
mantiki hiyo, ndiyo sababu kwa sasa kuna kushutumiana kwa hali ya juu kuhusu
majangili ni kina nani, wakati wanajulikana na hata kufikia hatua ya kuomba
kutajana kwa majina kwa wahusika humo humo bungeni.
Lililo
dhahiri na la kujiuliza ni kuwa: Je, ni kweli kwamba uhalifu wa
ujangili umepiga hodi bungeni kwa baadhi ya wabunge kujihusisha na uhalifu
huo tena kwa kutumia kofia za heshima na utukufu wa Bunge letu?
Hapa
sinuii kamwe kusema kuwa waheshimiwa wabunge au baadhi yao wanajihusisha na
uhalifu wa ujangili nchini, la hasha, lakini kinachosemwa na wao wanachosema,
wakiwa pia ni wananchi wana ndugu na marafiki zao ambao kuwatetea hao juu ya
ujangili kunazusha shaka kuwa utetezi huo si bure, bali huenda ni utetezi wa
kimasilahi.
Ndiyo
sababu habari zinazonukuliwa na vyombo vya habari ambazo hazijakanushwa pia
zinasema: ‘Ujangili kulitesa Bunge’, ndipo najiuliza kulitesa kwa vipi? Hivi
majangili wamo bungeni?
Jibu la
swali la maoni haya laweza kuwa jepesi au gumu kwa kuwa yawezekana likajibiwa
‘ndiyo’ au likajibiwa ‘hapana’ pasipo kutaka kuzingatia takwimu za waliosema
ndiyo au hapana. Lipo tatizo.
La
muhimu kuzingatia hapa ni kuwa, hakika hatuna budi kuwa makini sana kwani
Watanzania walio wengi kwa sasa si wale wa miaka ya 47, wanao upeo wa juu wa
uelewa na wenye ufahamu wa kutosha kabisa, hivyo watambuzi na wadadisi wa
kufahamu na kutambua mambo yao muhimu ya kitaifa na hali mbalimbali zenye
mushkeli na zinazopelekwa kimzaha na kwa mazoea.
Ni
mtazamo wangu kuwa huenda katika suala la ujangili ambalo ni moja ya tuhuma
za makosa ya jinai linapobainika na kutolewa taarifa hususan hata kuwepo
watuhumiwa waliokamatwa haipendezi kuona na kusikia utetezi mkubwa na mzito
namna ile bungeni huku hata wabunge wenyewe wakianza kutuhumiana hadharani
kuwafahamu wahusika.
Ni bora
tukapingana na tukaparaganyika ovyo katika masuala ya itikadi za vyama kwa
ngazi yake husika, lakini inapofika kwenye ngazi ya masuala ya masilahi ya
kitaifa hatuna budi kuachana na tofauti zetu za itikadi za vyama na kuwa kitu
kimoja (Bunge moja) kwa masilahi ya taifa.
Hakika
ujangili ni janga kwa utalii wetu na ukichezewa chezewa kimzaha na kimazoea
hivi hivi hakuna mnyama atakayesalimika nchini kwani mifano ipo mingi.
![]() Maoni: 0758 999 777. |
No comments:
Post a Comment