Charles Ndagulla-Tanzania daima
OKTOBA 13, mwaka huu ni siku iliyovuruga mwenendo
wa maisha ya kila siku ya wananchi wa Kijiji cha Minziro kilichopo Kata ya
Minziro, Wilaya ya Misenyi mkoani Kagera baada ya kundi la wanajeshi
wanaoendesha Operesheni Tokomeza Ujangili kuvamia kijiji hicho.
Kabla ya mkasa huo, siku hiyo ilikuwa tulivu.
Waumini wa madhehebu mbalimbali waliamka asubuhi na mapema kwenda kumwabudu
muumba wao kama ilivyo ada kila Jumapili.
Wakati waumini hawa wakirejea majumbani baada ya
kutoka kwenye ibada, walikutana na upepo mbaya, na huu si ule unaoezua mapaa
ya nyumba wala kung’oa miti, bali ni wa kipigo kutoka kwa walinda amani wetu.
Kila mmoja alikimbia kivyake kuokoa nafsi yake,
na wale walioshindwa kuhimili mikiki ya mbio waliangukia mikononi mwa
wapiganaji wetu, na hapo ndipo vipigo vilianza bila kuangalia sehemu ya
kupiga.
Makamanda hawa hawakuishia kutembeza vichapo kwa
raia wema tu, bali walienda mbali kwa kuchoma moto baadhi ya nyumba za
wananchi hao. Hakika Minziro iligeuka uwanja wa vita.
Wananchi hawa hadi sasa wamejawa na hofu,
hawamwamini mtu yeyote wasiyemfahamu, na kila wamuonapo wanajificha kwenye
mashamba ya migomba na baadhi yao vichakani wakitafakari kitakachotokea tena
kwa siku hiyo.
Ni wachache waliothubutu kuwasogelea wanahabari
waliotinga kijijini hapo kupata taarifa sahihi juu ya mkasa huo, lakini bado
walikuwa wamejawa na hofu hadi hapo walipotolewa hofu hiyo na wenyeji walioambatana
na wageni hao.
Mwenyekiti wa Kitongoji cha Mulungu A, Boniface
Ponsian, ambaye ni mmoja wa wahanga wa tukio hilo baada ya kukamatwa na
kushitakiwa kwa madai ya kumiliki mazao ya misitu bila kibali, anasema hali
bado ni tete kijijini hapo.
Anasema hadi sasa wananchi wengi wameyahama
makazi yao na kukimbilia mafichoni, huku wakiwaacha watoto wadogo wakiwa
hawana msaada wa wazazi wao.
Katika tukio hilo, wanajeshi hao wanadaiwa
kuwafunga kamba wananchi na kuwaning’iniza kwenye magari yao wakiwa wamewainamisha
vichwa chini, huku baadhi yao wanadaiwa kutapika kutokana na mtikisiko wa
magari.
Kwa mujibu wa mwenyekiti huyo, zaidi ya wananchi
20 wa Kijiji cha Minziro waliumizwa vibaya na askari hao wanaodaiwa kuwapa
mateso ya kila aina wakiwahusisha na wahamiaji haramu kutoka nchi za Burundi,
Rwanda na Uganda na uvunaji wa mazao ya misitu kutoka msitu wa hifadhi ya
taifa wa Minziro.
Kwa mujibu wa mwenyekiti huyo wa kitongoji,
wanajeshi hao baada ya kutembeza kipigo kwa wananchi kwa siku mbili
mfululizo, walichoma moto nyumba yakiwamo maduka na kubomoa baadhi ya milango
ya nyumba hizo.
Mwenyekiti huyo amewataja baadhi ya wahanga
walioshambuliwa na askari hao kuwa ni Josephat Joseph, Edwin George, Didas
Domisheni, Steven Serapioni, Sonko Yoronimu, Mkasa Mathias na Josephat
Emmanuel.
Wanajeshi hao walichoma moto duka la
mfanyabiashara Joseph Jovin wa Kijiji cha Minziro ambaye amekimbia makazi
yake sanjari na Edward Mgowa ambaye alibomolewa milango ya nyumba yake na
mwenyewe amekimbilia kusikojulikana yeye na mkewe na kuacha watoto wao watano
wakiwa wapweke.
Katika tukio hilo, askari hao walimuumiza
Josephat Emmanuel baada ya kupewa adhabu ya kutembelea magoti kwa umbali
mrefu.
Pamoja na ukweli kwamba vyombo vya ulinzi na
usalama Wilaya ya Misenyi vinafahamu operesheni hiyo, Mkuu wa Wilaya ya
Misenyi, Kanali mstaafu Issa Njiku, anadai hana taarifa yoyote juu ya tukio
hilo.
Kwa mtu wa kawaida, anaweza akahisi mkuu
hyo wa wilaya haelewi wajibu wake, lakini ukweli ni kwamba anaficha uoza
uliofanywa na walinzi hao wa amani ama kwa makusudi ama kwa kutokufahamu.
Si mkuu wa wilaya pekee, hata Kamanda wa Polisi
Mkoa wa Kagera, Phillp Kalangi naye usemi wake ni huo huo wa DC Njiku, kwamba
hana taarifa kutoka kwa OCD wake wa Misenyi, Yusuf Mtatifikolo, juu ya tukio
hilo ikiwa ni wiki tatu zimepita tangu litokee.
Tukio hilo halikuishia siku moja, liliendelea
siku ya pili ya Oktoba 14, ambako viongozi wa serikali ya kijiji hicho
walikamatwa na kuwekwa mahabusu polisi kwa siku tano kabla ya kufikishwa
mahakamani na kuhukumiwa ndani ya siku mbili.
Viongozi hao ni Mwenyekiti wa Kijiji cha Minziro,
John Sali Kilibwa, Mwenyekiti wa Kitongoji cha Mulungu A, Ponsian na
Anastazia Nestory ambao walihukumiwa Oktoba 22, mwaka huu kwenda jela miaka
miwili au kulipa faini ya sh milioni moja kila mmoja baada ya kupatikana na
hatia ya kumiliki mazao ya misitu bila kibali. Walilipa faini.
Wakati viongozi hao wakinusurika kwenda gerezani
kutumikia kifungo, mwalimu mkuu wa Shule ya Msingi Minziro, yeye alikwenda
gerezani baada ya kujikuta akikamatwa muda mfupi tu baada ya kuwatolea
ushahidi viongozi hao wa kijiji. Amefunguliwa mashitaka matatu; kuvuna mazao
ya misitu bila kibali, kusafrisha mazao ya misitu bila kibali na kumiliki
mazao ya misitu kinyuume cha sheria. Kesi yake bado inaendelea.
Kwa muundo wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya
Mkoa, Mkuu wa Mkoa, Kanali mstaafu Massawe, ndiye mwenyekiti wake na katibu
ni Mkuu wa Usalama wa Taifa wa Mkoa (RSO). Ndivyo hivyo na wilayani ambako DC
Njiku ni mwenyekiti wa kamati na katibu wake ni DSO.
Mbali na wanajeshi, wengine waliokuwa
wakitekeleza operesheni ya kuwashambulia wananchi wa Kijiji cha Minziro na
vitongoji vyake wanatoka kwenye Idara ya Usalama wa Taifa, polisi na
maofisa kutoka Idara ya Misitu ambayo kwa sasa inaitwa Wakala wa Huduma za
Misitu Tanzania.
Swali ni je, nani atawaondolea hofu na mashaka
wananchi hao wa Kijiji cha Minziro na vitongji vyake pamoja na vijiji jirani?
Kwani hadi naandika makala hii, wanajeshi hao wangali wakivinjari kijijini
hapo wakiwasaka watu waliowaumiza wenyewe kwa sababu wanazozifahamu wenyewe.
ndagullacharles@yahoo.com
078
|
No comments:
Post a Comment